KAMA MWANAUME HAHUDUMII FAMILIA ACHA KIHEREHERE CHA KUBEBA MAJUKUMU YAKE IPO SIKU YATAKUSHINDA! - EDUSPORTSTZ

Latest

KAMA MWANAUME HAHUDUMII FAMILIA ACHA KIHEREHERE CHA KUBEBA MAJUKUMU YAKE IPO SIKU YATAKUSHINDA!

Image result for housegirl kicheche
Nimeamue nitumie maneno makali kwani naona namna ambavyo wanawake wengi wanapoingia kwenye ndoa huona kama ni kawaida kubeba majukumu ya mume lakini mambo yakiwashinda huanza kulalamika na kusema kuwa wametelekezewa familia. Nianze kwa kusema, unapoolewa ni jukumu la mume wako kukuhudumia kwa kila kitu wewe na wanao na kama hawezi abaki tu msela si lazima kuoa, sabuni ni bei rahisi zaidi!
Hainogi na ndoa haitadumu kama mwanaume unahudumiwa na mwanamke, ukubali usikubali ndiyo hivyo, mwanaume aliyekamilika hawezi kuhudumiwa kila kitu na mkewe. Sasa msinielewe vibaya maisha nikusaidiana na kama mke ana kipato kikubwa basi suala la kumsaidia mume ni la lazima, narudia nilalazima lakini hapa neno ni “KUSAIDIANA” na si “KUBEBA MAJUKUMU” sijui kama mmenipata mke anatakiwa asaidie.
Sasa narudi kwenye “KIHEREHERE” hapo juu, wanawake wengi wakiwa na kazi, wanakipato kuna kakitu wanasema “Mimi siwezi kuombao omba kama yeye hajui majukumu yake ni yeye!” Hapa mwanamke anafanya majukumu yote, analipa kodi, ananunua chakula, anahudumia watoto na kila kitu na haoni shida. Mume yeye zake anaishia kununulia Bia au kuhonga na akirudi anataka chakula na maji ya kuoga.
Sasa hii haina shida katika ndoa changa, hapa unakuta kwanza labda mko wawili tu, au kama mna watoto ni wachanga na hata kama ni wakubwa hawasomi. Lakini kama ni kusoma ni mmoja tu au wawili, hivyo mwanamke anawamudu. Anahudumia na haoni shida au hata kama anaona shida lakini si ana uwezo na anaona tabu kuomba.
Ila kimbembe Dada yangu kinakuja pale watoto wamekua wakubwa, una watoto wawili watatu wanaosoma shule ada milioni kadhaa, wanahitaji kuvaa, kula na kila kitu. Mume ndiyo huyo ulishamfanya bwege hawazi tena majukumu, si mke ana kazi bwana na alishazoea hata asipotoa matumizi akirudi anakula na kufoka kabisa, hapo ndiyo unachanganyikiwa kwani majukumu yamezidi.
Mume ukimuambia ashazoea kusema hana na kwakua anajua akisema hana wewe utalipa ada tu basi anaacha kabisa, mwanamke unaanza kuchakaa kwa mawazo, badala uwaze mambo ya Brazilian na Gucci unawaza kulipa ada! Unamlaumu mwanaume kakutelekezea watoto kumbe kiherehere chako cha huko nyuma kujifanya huwezi kuomba hela, kujifanya unavihela ndiyo kinakuponza.
Najua mkiambiwa kwa upole hamsikii mnaanza Kusema “Sasa kama hatoi mimi nifanye nini?” Mimi nasema acha kiherehere, kama kakuoa na hataki kutoa hela ya chakula hata kama unafanya kazi Benki ya dunia hembu pika chakula chako na wanao mle akirudi muambie kabisa hela uliyokua nayo haikutosha. Kama halipi bili ya umeme Mama aje akutane na giza na kama halipi kodi ndugu yangu basi vyombo vitolewe nnje.
Narudia hata kama una hela acha kiherehere, sijakosea nasema acha kiherehere cha kufanya kila kitu. Kama ni watoto hataki kulipa ada aje awakute hawajaenda shule na jifanye kama hujali hata kama unajali. Kitu pekee ambacho huwezi kukifanya ni kuwanyima wanao chakula, hapana ila vingine ambavyo haviui usifanye, mumeo anatakiwa kujua kuwa yeye ndiyo kakuoa na si wewe.
Hapa nataka mnielewe pia, kuna wakati mwanaume mambo yanakua magumu, hapa hata wewe unaona na hutakiwi kumnyanyasa na beba majukumu. Ila kama ana kazi, mambo wala si magumu ila hela yake huioni jua anaenda kuihongea hembu acha ujinga wa kulea mtu mzima, kama alikua bado hajaweza kujitegemea kwanini aoe, si arudi kwenda kunyonya kwa Mama yake.
Lakini pia hata hapa msichanganye, kuna ambao hawana kazi lakini hata hawajiongezi, kwamba hana kazi lakini kutwa kucha anachezea rimoti tu na watoto na kusubiri maji ya kuoga. Si mke ana kazi yeye wala hata hajikuni. Ukimpa mtaji wa biashara anaenda kuhonga na akirudi anataka matumizi kabisa. Mwingine ukimnyima au ukimuambia huna analalamika na kununa kabisa.
Anajifanya kuongea kwa mafumbo kuwa unamnyanyasa na kujifanya mnyongeeee utafikiri yuko kwenye Bleed! Kama ni wa aina hii basi jua anakuchukulia poa na kashakuona kama mume wake! Dada yangu acha kumuendekeza, punguza matumizi mpaka ajiongeze na kutafuta kazi ya kufanya, kumbuka mwanamke anaweza kuwa Mama wa nyumbani ila mwanaume hawezi kuwa Baba wa nyumbani!
Mnatia hasira sana Dada zangu, wengi wenu mnaolalamika kutelekezewa familia nikwakua mnajifanya hamjui kuomba mnabeba majukumu. Mwanaume hawezi kukutelekezea watoto kama hajui kama una namna ya kuwahudumia, lakini utamlishaje mwanaume mtu mzima. Badilika na kuwa mke, acha kubeba majukumu yake sasa, unaona ni madogo ila hao watoto wakikua utachanganyikiwa na kiherehere chako acha!




Download our APP from Google Playstore using the link here>>>

Join Our Telegram Channel for Daily Updates CLICK HERE

No comments:

Post a Comment

Edusportstz